Maadhimisho ya Siku ya Sheria Wilaya ya Ruangwa yamefanyika leo tarehe 02 katika Ukumbi wa Mahakama ya Wilaya ya Ruangwa, yakihusisha wadau mbalimbali wa sheria, viongozi wa serikali, pamoja na wananchi wa wilaya hiyo.
Mgeni rasmi katika maadhimisho hayo alikuwa Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa, Hassan Ngoma, ambaye alisisitiza umuhimu wa Mahakama kama muhimili muhimu katika ustawi wa jamii, maendeleo ya kiuchumi ya nchi na kukuza uwekezaji.
Akizungumza wakati wa maadhimisho hayo, Mheshimiwa Ngoma alisema kuwa Mahakama ina nafasi kubwa katika kudumisha haki, amani na utulivu katika jamii, jambo ambalo ni msingi muhimu wa maendeleo endelevu. Alibainisha kuwa uwepo wa mifumo madhubuti ya haki huongeza imani ya wananchi na wawekezaji, hivyo kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika ngazi ya wilaya na taifa kwa ujumla.
“Mhimili wa Mahakama ni nguzo muhimu katika ustawi wa jamii na maendeleo ya nchi. Bila haki na usawa, hakuna maendeleo ya kweli yanayoweza kupatikana,” alisema Mheshimiwa Ngoma.
Aidha, aliwataka wananchi kuendelea kuitumia Mahakama kama chombo halali cha kutatua migogoro yao, badala ya kujichukulia sheria mkononi, huku akiwahimiza watumishi wa Mahakama kuendelea kutoa huduma kwa uadilifu, uwazi na kwa kuzingatia misingi ya haki.
Maadhimisho ya Siku ya Sheria hufanyika kila mwaka nchini kwa lengo la kutathmini utekelezaji wa majukumu ya Mahakama, kuimarisha uelewa wa wananchi kuhusu haki zao za kisheria, pamoja na kuhimiza mshikamano kati ya Mahakama na jamii.
Ruangwa
Anuani ya Posta: S.L.P 51
Simu ya Mkononi: 0732932312
simu: 0732932312
Barua pepe: ded@ruangwadc.go.tz
Hatimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa