Maonesho ya Madini na Fursa za Uwekezaji Mkoa wa Lindi 2025 yamefungwa rasmi leo tarehe 14 Juni katika Viwanja vya Maonesho Kilimahewa, Wilayani Ruangwa.
Tukio hilo kubwa limefungwa na Naibu Waziri wa Madini, Mhe. Dkt. Steven Kiruswa (Mb.) kwa niaba ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Ruangwa.
Akizungumza wakati wa kufunga maonesho hayo, Mhe. Dkt. Kiruswa ameeleza kuwa Serikali itaendelea kusimama bega kwa bega na wachimbaji wadogo na wawekezaji wa ndani na nje ili kuhakikisha rasilimali za madini zinawanufaisha wananchi wote.
“Tunapenda kuona wananchi wa Lindi na Tanzania kwa ujumla wakifaidika moja kwa moja na rasilimali hizi. Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji na kuwezesha wachimbaji wadogo kupiga hatua zaidi,” amesema Dkt. Kiruswa.
Kwa upande mwingine, Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe. Zainab Telack, amewapongeza waandaaji, wadau, na wananchi kwa kujitokeza kwa wingi, akisisitiza kuwa maonesho hayo ni sehemu ya mapinduzi ya kiuchumi kwa Mkoa wa Lindi.
“Lindi siyo tena Mkoa wa kusubiri, sasa tunasonga mbele kwa vitendo. Maonesho haya yamedhihirisha kuwa tunaweza kujenga uchumi imara kwa kutumia fursa zetu za ndani, hususan katika madini,” amesema Mhe. Telack.
Aidha, kwa siku nne mfululizo (11–14 Juni), zaidi ya mabanda 120 yaliwekwa na kuendeshwa na wachimbaji wadogo, taasisi za umma, mashirika binafsi, wajasiriamali na watoa huduma mbalimbali katika mnyororo wa thamani wa sekta ya madini.
Mbali na hayo, mwaka huu maonesho yaliambatana na kauli mbiu:
“Madini na Uwekezaji: Fursa ya Kiuchumi Lindi – Shiriki Uchaguzi Mkuu 2025.”
Vilevile, zaidi ya asilimia 75 ya uendeshaji wa maonesho uligharimiwa na wadhamini wakubwa kama Ellianje Genesis, Lindi Jumbo, MAST, UVIWAMA, PMBet, pamoja na makampuni, taasisi na watu binafsi zaidi ya 50.
Kwa ujumla, Kwa ujumla, maonesho haya yametoa dira mpya kwa uchumi wa mkoa, kuleta hamasa kwa wachimbaji wadogo, na kuongeza mwamko wa wananchi kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo.
Ruangwa
Anuani ya Posta: S.L.P 51
Simu ya Mkononi: 0732932312
simu: 0732932312
Barua pepe: ded@ruangwadc.go.tz
Hatimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa