

Katibu Tawala wa Mkoa wa Lindi, Bi. Zuwena Omary, amewataka Maafisa Habari wa Halmashauri zote za Mkoa huo kuimarisha uhusiano wa karibu na vyombo vya habari, ili kuhakikisha taarifa za Serikali zinawafikia wananchi kwa haraka, kwa usahihi na kwa uwazi.
Akizungumza katika kikao kazi kilichofanyika leo tarehe 5 Februari 2026 katika Ukumbi Mdogo wa Mikutano uliopo Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Bi. Omary amesema kuwa mahusiano mazuri kati ya Maafisa Habari na waandishi wa habari ni msingi wa kujenga uaminifu wa umma na kuimarisha taswira ya Serikali.
Amesisitiza kuwa kwa kushirikiana na vyombo vya habari kwa uwazi, kwa kuheshimiana na kwa kutoa taarifa kwa wakati, Serikali itaweza kuifikia jamii kwa ufanisi zaidi na kuhamasisha ushiriki wa wananchi katika shughuli za maendeleo.
“Vyombo vya habari ni wadau muhimu. Mnapoimarisha uhusiano nanyi, mnaimarisha mawasiliano ya Serikali kwa wananchi,” amesema Bi. Omary.
Aidha, amewahimiza Maafisa Habari kutumia vyombo vya habari kama daraja la kutangaza fursa za uwekezaji, miradi ya maendeleo na mafanikio ya Mkoa wa Lindi bila kusahau kutumia vizuri tovuti na mitandao ya kijamii ya Halmashauri zao.
Kikao hicho kimewakutanisha Maafisa Habari kutoka Halmashauri zote za Mkoa wa Lindi, kikilenga kuimarisha ushirikiano na kujadili mbinu bora za kujenga mahusiano endelevu kati ya Serikali na vyombo vya habari.
Ruangwa
Anuani ya Posta: S.L.P 51
Simu ya Mkononi: 0732932312
simu: 0732932312
Barua pepe: ded@ruangwadc.go.tz
Hatimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa