Maelfu ya wananchi na wadau wa sekta ya madini wamejitokeza kwa wingi leo Juni 11, 2025, katika Viwanja vya Madini vilivyopo Kilimahewa, wilayani Ruangwa kushuhudia uzinduzi rasmi wa Maonesho ya Madini Mkoa wa Lindi – (Lindi Mining Expo 2025.)
Mgeni rasmi katika uzinduzi huo amekuwa Mhe. Shaib Hassan Kaduara, Waziri wa Maji Nishati na Madini kutoka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, ambaye amesisitiza umuhimu wa ushiriki wa wadau wote katika kuchochea uchumi wa madini kupitia ushirikiano wa kitaifa na kimataifa.
Aidha, katika hotuba yake Mhe. Kaduara amesema wananchi wanawajibu wa kulinda na kusimamia vizuri urithi wa madini yanayopatikana nchini. “Madini ni urithi wetu wa pamoja tukiyasimamia kwa umoja, yataleta mabadiliko ya kweli katika maisha ya wananchi wetu.” Amesema Mhe. Kaduara
Maonesho hayo ya siku nne, yanatarajiwa kufikia tamati Juni 14, 2025, yamewakutanisha wachimbaji wakubwa na wadogo, wawekezaji wa ndani na nje ya nchi, watafiti, taasisi za kifedha, wataalamu wa mazingira, pamoja na wananchi wanaotafuta fursa za kiuchumi kupitia sekta ya madini.
Kwa kuzingatia mwelekeo wa maonesho hayo, kauli mbiu ya mwaka huu ni: “Madini na Uwekezaji, Fursa ya Kiuchumi Lindi – Shiriki Uchaguzi Mkuu 2025”, ikisisitiza umuhimu wa rasilimali za madini katika kuchochea maendeleo ya Mkoa huku ikihamasisha ushiriki wa wananchi kwenye masuala ya kijamii na kidemokrasia.
Hata hivyo, maonesho haya yanatarajiwa kutoa jukwaa la kukuza uelewa, kuanzisha ushirikiano wa kibiashara na kuwezesha mnyororo wa thamani wa madini kufikiwa na wananchi wa kawaida – ikiwa ni sehemu ya ajenda pana ya Serikali za Mikoa na Serikali Kuu kuimarisha uchumi wa rasilimali.
Ruangwa
Anuani ya Posta: S.L.P 51
Simu ya Mkononi: 0732932312
simu: 0732932312
Barua pepe: ded@ruangwadc.go.tz
Hatimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa