Watumishi wa Mkoa wa Lindi wametakiwa kutumia ipasavyo fursa ya ushiriki wao katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma Kitaifa kwa mwaka 2025 ili kujifunza na kuboresha utendaji wa kazi katika maeneo yao.
Wito huo umetolewa Juni 22, 2025 na Katibu Tawala wa Mkoa wa Lindi, Bi. Zuwena Omary, alipotembelea viwanja vya Chinangali Jijini Dodoma ambako maadhimisho hayo yanaendelea tangu Juni 16 na yanatarajiwa kufungwa rasmi Juni 23, 2025.
Akizungumza katika ziara hiyo, Bi. Zuwena amesema kuwa ushiriki katika maadhimisho hayo ni muhimu kwa sababu unawapa watumishi nafasi ya kuona na kujifunza mbinu bora kutoka taasisi na ofisi nyingine. Aidha, amesisitiza kuwa kujifunza kutoka kwa wengine ni njia mojawapo ya kuongeza ufanisi wa utendaji kazi serikalini.
Sambamba na hilo, Katibu Tawala huyo amewapongeza watumishi wa Mkoa wa Lindi kwa ubunifu waliouonesha katika mabanda yao na ushiriki wao hai katika kuwakilisha Mkoa kwa mafanikio.
Awali, Katibu Tawala Msaidizi (Utawala), Ndg. Nathalis Linuma, ametoa taarifa fupi kuhusu ushiriki wa Mkoa wa Lindi, akibainisha kuwa Halmashauri zote za Mkoa huo zimeonesha miradi bunifu katika utoaji wa huduma. Kwa mfano, Halmashauri ya Nachingwea imewasilisha huduma ya “One-Stop Centre”, Halmashauri ya Mtama imeonesha mfumo wa kidigitali wa utunzaji misitu na uvunaji wa hewa ukaa, huku Hospitali ya Mkoa ikiwa imewasilisha “Kadi_Alama”, mfumo unaosaidia kufuatilia utendaji kazi.
Mbali na hayo, Bi. Zuwena amepewa fursa ya kutembelea mabanda mbalimbali kama TPDC, ambako ameangalia video ya utekelezaji wa mradi wa gesi asilia (LNG) unaotarajiwa kufanyika mkoani Lindi. Vilevile, ametembelea mabanda ya EWURA, LATRA, TFS, na Mbeya RS, ambako amepata elimu mbalimbali ikiwemo tiba asilia ya kudungwa na nyuki.
Kwa upande mwingine, watumishi wa Mkoa wa Lindi wametumia nafasi hiyo kumshukuru Katibu Tawala kwa kuwezesha ushiriki wao kwenye maadhimisho hayo na kwa kuandaa mazingira rafiki yaliyowawezesha kujifunza na kushirikiana kitaaluma na watumishi kutoka maeneo mbalimbali nchini.
Ruangwa
Anuani ya Posta: S.L.P 51
Simu ya Mkononi: 0732932312
simu: 0732932312
Barua pepe: ded@ruangwadc.go.tz
Hatimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa