Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa, Mhe. Hassan Ngoma, ameshiriki hafla ya uzinduzi wa ugawaji wa mikopo ya asilimia kumi kwa vikundi vya Wanawake, Vijana na Watu wenye Ulemavu, ikiwa ni sehemu ya mpango wa uwezeshaji wananchi kiuchumi kupitia asilimia kumi (10%) ya mapato ya Halmashauri.
Hafla hiyo imefanyika leo tarehe 18 Februari, 2026 katika bwalo la Shule ya Sekondari Ruangwa Girls na kuhudhuriwa na viongozi na wadau mbalimbali wakiwemo Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa, Katibu Tawala wa Wilaya, Katibu wa Chama Cha Mapinduzi Wilaya, Katibu wa Mbunge, Wakuu wa Idara na Vitengo, pamoja maafisa wa TAKUKURU na wawakilishi wa taasisi za kifedha (NMB Bank)
Akiwasilisha taarifa ya utoaji wa mikopo hiyo, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri, Mwl. George Mbesigwe, amesema kuwa katika robo ya pili ya mwaka wa fedha 2025/2026, Halmashauri imetoa jumla ya shilingi 420,877,000 kwa vikundi 71 vya makundi maalum. Kati ya fedha hizo, vikundi 37 vya wanawake vyenye wanufaika 198 vimekopeshwa shilingi 164,636,000. Vikundi 24 vya vijana vyenye wanufaika 130 wanaume 113 na wanawake 17 vimekopeshwa shilingi 232,541,000. Aidha, vikundi 10 vya watu wenye ulemavu vyenye wanufaika 15, wanawake 3 na wanaume 12, vimekopeshwa shilingi 23,700,000.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mkuu wa Wilaya Mhe. Ngoma amesema, "Mikopo hii ya asilimia kumi ni fursa muhimu ya kuwawezesha wananchi kiuchumi. Ni wajibu wa kila kikundi kuitumia kwa malengo yaliyokusudiwa, kuendesha miradi yenye tija na kurejesha kwa wakati ili na wengine wapate kunufaika. Nidhamu ya fedha ndiyo itakayofanya mpango huu ulete matokeo halisi katika maendeleo ya Ruangwa".
Kwa upande wao wanufaika wa mikopo hiyo wametoa shukrani kwa Serikali kwa kuwawezesha mitaji ya kuanzisha na kukuza miradi ya kiuchumi, wakiahidi kutumia fedha hizo kwa malengo yaliyokusudiwa na kuzirejesha kwa wakati.
Ruangwa
Anuani ya Posta: S.L.P 51
Simu ya Mkononi: 0732932312
simu: 0732932312
Barua pepe: ded@ruangwadc.go.tz
Hatimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa