Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa, Ndugu Frank Fabian Chonya, amesema kuwa Halmashauri hiyo inakaribia kupata hadhi ya Manispaa kutokana na kasi ya maendeleo yanayoendelea kushuhudiwa katika maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo.
Akizungumza usiku wa kuamkia Mei 21, 2025, kwenye sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Wauguzi Duniani zilizofanyika katika Ukumbi wa Ruangwa Pride Hotel, Ndugu Chonya ambaye alikuwa mgeni rasmi amesema hatua hiyo ni matokeo ya juhudi kubwa za Serikali na ushirikiano wa wananchi katika kuchochea maendeleo.
“Kama mnavyoona, Ruangwa inabadilika kwa kasi. Ujenzi wa miundombinu, huduma bora za kijamii, na upanuzi wa mji, yote haya ni viashiria kuwa Ruangwa inaelekea kuwa Manispaa muda si mrefu,” amesema Ndugu Chonya.
Aidha, amewapongeza wauguzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa kwa kuadhimisha siku yao kwa namna ya kipekee na kuwataka waendelee kuwa na weledi na kujituma katika kuhudumia wananchi.
Ameongezaa kuwa, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeendelea kuboresha mazingira ya kazi na maslahi ya watumishi wa afya na sekta nyingine, hivyo ni wajibu wa watumishi hao kulipa hilo kwa kufanya kazi kwa bidii na uadilifu.
Katika hotuba yake, Ndugu Chonya amemshukuru Mbunge wa Jimbo la Ruangwa ambaye pia ni Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa, kwa mchango wake mkubwa katika maendeleo ya Ruangwa na mwelekeo wake wa kuwa mji wa kisasa.
Kwa upande wao, wauguzi wa Wilaya ya Ruangwa wameushukuru uongozi wa Halmashauri kwa kuwaunga mkono katika majukumu yao ya kila siku, na wameahidi kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi kwa kuzingatia maadili ya taaluma yao.
Maadhimisho ya Siku ya Wauguzi Duniani, ambayo hufanyika kila Mei 12, hutumika kama jukwaa la kutambua mchango mkubwa wa watumishi wa afya katika jamii na kuwakumbusha nafasi yao muhimu katika kuboresha maisha ya wananchi.
Ruangwa
Anuani ya Posta: S.L.P 51
Simu ya Mkononi: 0732932312
simu: 0732932312
Barua pepe: ded@ruangwadc.go.tz
Hatimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa