Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa imetajwa kuwa ya 13 kitaifa kwa ufaulu wa Mtihani wa Darasa la Saba (PSLE) mwaka 2024, kwa mujibu wa vigezo vya Viashiria Muhimu vya Utendaji (Key Performance Indicators - KPIs), ikihusisha shule za Serikali pekee.
Taarifa hiyo imetolewa leo tarehe 20 Juni 2025, ikiwa ni matokeo ya jitihada endelevu zinazofanywa na Halmashauri hiyo katika kuboresha sekta ya elimu ya msingi.
Aidha, katika kutambua mchango mkubwa uliowezesha mafanikio hayo, Afisa Elimu wa Awali na Msingi wa Wilaya ya Ruangwa, Mwl. George Mbesigwe, amekabidhiwa cheti maalum kama ishara ya pongezi na kutambua juhudi za Halmashauri katika kuimarisha usimamizi wa taaluma shuleni.
Vilevile, cheti hicho ni sehemu ya motisha kwa viongozi wa elimu ngazi ya Wilaya wanaoonesha matokeo chanya katika kuinua viwango vya ufaulu, hasa kwa kuzingatia vigezo vya kitaifa vya tathmini ya utendaji.
Halikadhalika, nafasi hii ya 13 kitaifa inaiweka Ruangwa katika orodha ya Halmashauri zinazofanya vizuri nchini, na hivyo kuwa kielelezo cha mafanikio ya uwekezaji wa Serikali kwenye elimu ya msingi kupitia uimarishaji wa miundombinu, vifaa vya kujifunzia na mazingira bora ya kufundishia.
Kwa ujumla, mafanikio haya yanadhihirisha mshikamano baina ya walimu, wazazi, wanafunzi na uongozi wa elimu katika kuhakikisha watoto wanapata elimu bora na yenye tija.
Ruangwa
Anuani ya Posta: S.L.P 51
Simu ya Mkononi: 0732932312
simu: 0732932312
Barua pepe: ded@ruangwadc.go.tz
Hatimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa