Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru 2025, Ndugu Ismail Ali Ussi, ameizindua rasmi mradi wa maji safi na salama katika Kijiji cha Mpara Kata ya Likunja wenye thamani ya Shilingi Milioni 325, uzinduzi huo umefanyika leo tarehe 28 Mei 2025 mbele ya wananchi, viongozi wa kijiji na wataalam wa Sekta ya maji.
Mradi huo unajumuisha uchimbaji wa visima vitano pamoja na ujenzi wa miundombinu rahisi ya maji katika vijiji vya Mmawa, Njawale, Mtawilile, Mpara na Namkatila, umeghalimu shilingi 325,000,000.00 ukiwa ni mkombozi mkubwa kwa wakazi waliokuwa wanatembea umbali mrefu kufuata huduma hiyo muhimu.
Akizungumza wakati wa kuzindua mradi huo, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru, Comrade Ismail Ussi, amesema kuwa upatikanaji wa maji safi ni haki ya msingi kwa kila Mtanzania, na kwamba serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha huduma hiyo inafika maeneo yote ya vijijini.
“Mradi huu ni ushahidi wa dhamira ya serikali katika kuhakikisha wananchi wa maeneo ya vijijini hawabaki nyuma kwenye maendeleo. Maji ni uhai, na kupatikana kwake kwa urahisi ni hatua kubwa kuelekea ustawi wa jamii,” amesema Comrade Ussi.
Mwenge wa Uhuru 2025 unaendelea na ziara yake mkoani Lindi kwa lengo la kukagua, kuzindua na kuweka mawe ya msingi katika miradi ya maendeleo, huku ukiendelea kuhimiza ushiriki wa wananchi katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu kwa njia ya amani na utulivu.
Kwa ujumla, uzinduzi huo umepongezwa na wananchi wa kijiji cha Mpara na maeneo jirani, waliomshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kusogeza huduma za msingi karibu na wananchi kupitia miradi ya maendeleo inayoendeshwa kwa ushirikiano na wadau mbalimbali.
Kaulimbiu ya Mbio za Mwenge wa Uhuru 2025 inasema: “Jitokeze Kushiriki Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 kwa Amani na Utulivu.”
Ruangwa
Anuani ya Posta: S.L.P 51
Simu ya Mkononi: 0732932312
simu: 0732932312
Barua pepe: ded@ruangwadc.go.tz
Hatimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa