Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa Mhe. Hassan Ngoma amezindua rasmi zoezi la ugawaji wa miche bora ipatayo 175,701 ya mikorosho kwa wakulima waliosajiliwa na Ofisi ya Kilimo, kata na vijiji Wilayani humo, ikiwa ni utekelezaji wa mkakati wa kuongeza uzalishaji wa zao la korosho msimu wa 2025/2026.
Zoezi hilo limefanyika leo tarehe 19 Februari, 2026 katika vitalu vya uzalishaji miche ya mikorosho vilivyopo Kijiji cha Kilimahewa kata ya Nachingwea. Akizungumza katika hafla hiyo, DC Ngoma amesema ugawaji huo ni hatua ya kimkakati katika kuimarisha uchumi wa wananchi na kuongeza tija ya zao hilo ambalo ndilo tegemeo kuu la Wilaya ya Ruangwa.
“Korosho ni uti wa mgongo wa uchumi wa Wilaya yetu hivyo miche hii ikitunzwa vizuri itaongeza uzalishaji, kipato cha mkulima mmoja mmoja na mapato ya Halmashauri. Ni wajibu wetu kuhakikisha kila mche unapandwa na kuendelezwa kwa kuzingatia ushauri wa wataalamu wa kilimo,” amesema Mhe. Ngoma.
Katika taarifa yake Mkuu wa Idara Kilimo, Mifugo na Uvuvi Ndg. Thadei M. Luoga amebainisha kuwa lengo la Halmashauri kwa msimu huu lilikuwa kuzalisha miche 200,000, ambapo hadi sasa miche 175,701 imezalishwa kupitia vikundi saba(7) vya uzalishaji vilivyoingia mkataba na Bodi ya korosho ndani ya Wilaya na kuanza kugawiwa bure kwa wakulima waliosajiliwa rasmi.
Ameongeza kuwa Wilaya ya Ruangwa ina wakulima wa korosho 23,588 wenye miti 5,543,028 katika eneo la hekta 73,907. Zao la korosho linachangia zaidi ya asilimia 85 ya mapato ya wananchi. Katika mwaka wa fedha 2025/2026, zao hilo limeingizia Halmashauri zaidi ya shilingi bilioni 1.6, huku wakulima wakilipwa zaidi ya shilingi bilioni 80.1 kutokana na mauzo ya korosho ghafi.
Aidha, tathmini ya misimu minne kuanzia 2022/2023 hadi 2025/2026 inaonesha jumla ya miche 454,812 imezalishwa na kugawiwa kwa wakulima. Jumla ya ekari 5,856 zinatarajiwa kupandwa katika awamu hii, huku Ofisi ya Kilimo ikiendelea na usimamizi na ufuatiliaji wa upandaji na ukuaji wa miche hiyo ili kuhakikisha inaleta matokeo chanya yaliyokusudiwa.
Ruangwa
Anuani ya Posta: S.L.P 51
Simu ya Mkononi: 0732932312
simu: 0732932312
Barua pepe: ded@ruangwadc.go.tz
Hatimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa